Home » » Kibaha, Organia kuwekeza ufugaji wa kuku

Kibaha, Organia kuwekeza ufugaji wa kuku

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

SHIRIKA la Elimu Kibaha, limeingia makubaliano ya kisheria na Kampuni ya kimataifa ya Organia katika uwekezaji wa ufugaji wa kuku wa kisasa, utakaoliwezesha shirika hilo kuvuna Sh milioni 100 kwa mwaka na kutoa ajira kwa watu 700.
Akizungumza mara baada ya kutiwa saini kwa makubaliano hayo jana jioni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Hawa Ghasia, alisema uwekezaji huo unatarajiwa kuleta manufaa kwa shirika hilo kwani uwekezaji wake pia utasaidia kutoa elimu kwa vitendo juu ya ufugaji kwa kada mbalimbali.
Alisema miaka ya nyuma shirika hilo lilikuwa likisifika kwa ufugaji wa kuku kabla ya kusitisha shughuli hizo kutokana na uwepo wa sababu mbalimbali na kusababisha shirika hilo kukosa mapato yaliyokuwa yakitokana na uuzaji wa kuku na mayai.
Mkurugenzi wa Shirika la Elimu Kibaha, Cyprian Mpemba alisema uwekezaji huo wa miaka 66, mbali na kuingizia shirika hilo kiasi cha Sh milioni 100 kila mwaka, pia utawawezesha kuvuna kiasi kingine kama hicho kama ada ya uingiaji katika eneo hilo.
Alisema itachukua muda wa miaka nane hadi uwekezaji rasmi ukamilike katika eneo hilo ukihusisha idara mbalimbali ikiwemo ujenzi wa viwanda vya usindikaji wa nyama na utengenezaji wa soseji, huku kila baada ya miaka miwili wakikamilisha ujenzi wa eneo yakiwemo maeneo ya kufugia kuku hao.
Mpemba alisema matarajio baada ya mika miwili ijayo mradi huo utaweza kuzalisha kuku milioni 2.7 huku wakitoa ajira kwa watu 120 na ukikamilika utazalisha kuku milioni 165 pamoja na kutoa ajira kwa watu 700 hatua aliyosema itasaidia kuleta mapinduzi katika ufugaji wa kuku hapa nchini sambamba na kutoa elimu kwa wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali.
Naye Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo Hesham Ewies alisema malengo yao ni kuibadilisha Kibaha kwa muda mfupi kwa kulifanya kuwa eneo linalosifika kutokana na shughuli za ufugaji wa kuku huku zaidi wakilenga kuondoa upungufu wa mahitaji ya bidhaa ya kuku yaliyopo kwa sasa nchini.
Alisema watarajio yao baada ya miaka michache ijayo, Tanzania itaweza kusifika kwa usafirishaji wa bidhaa zitokanazo na kuku kwenda nje ya nchi na hivyo kuliongeza Taifa mapato.
Chanzo;Habari Leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa