Home » » POLISI: USALAMA PWANI WAREJEA KWA ASILIMIA 99

POLISI: USALAMA PWANI WAREJEA KWA ASILIMIA 99

Imeandikwa na Mwandishi Wetu
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Pwani, Jonathan Shanna
HALI ya usalama mkoani Pwani imeimarika kwa asilimia 99 kutokana na Polisi kudhibiti uhalifu. Kamanda wa Polisi mkoani humo, Jonathan Mshana alisema jana kuwa hivi sasa vyombo vya dola vinaendelea kusaka mabaki ya wahalifu hao kila kona nchini ili wawachukulie hatua za sheria.
“Naweza kusema uhalifu umekwisha na kufikia pointi sifuri. Tunaendelea kuvisaka vimelea vidogo vidogo vya wahalifu hao nyumba kwa nyumba popote walipo tutawapata,” alisema Kamanda Mshana.
Pasipo kutaja takwimu, Kamanda Mshana alisema matukio hayo ya uhalifu Pwani yaligharimu maisha ya viongozi na watendaji wa vijiji pamoja na askari lakini pia wahalifu nao walipoteza maisha.
Kutokana na watendaji wa vijiji kupoteza maisha na wengine sifa ya kuwa viongozi, Halmashauri za Wilaya ya Mkuranga na Kibiti zilitangaza nafasi za kazi kuziba nafasi hizo za watendaji zilizokuwa wazi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga, Mshamu Munde alisema nafasi 66 za watendaji wa kijiji zilizotangazwa Agosti mwaka huu zitazibwa rasmi wiki hii na watendaji wapya.
Munde alisema walipokea maombi zaidi ya 1,500 ya watu walioomba nafasi za watendaji wa kijiji. Alisema baada ya usaili, wiki hii watawaajiri waende wakaanze kazi katika vijiji watakavyopangiwa.
“Ajira hii ni ya kuziba nafasi za watendaji wa awali ambao wengi walipoteza sifa ya kuendelea kuwa watendaji wa vijiji kama kukosa elimu ya kidato cha nne, kuziba nafasi za watendaji waliopoteza maisha kutokana na mauaji,” alieleza Munde.
Alisema kupitia uhakiki wa watumishi wa umma, ilibainika watendaji 66 hawakuwa na sifa kwa kukosa elimu ya kidato cha nne na kupoteza ajira zao. Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti, Alvera Ndabagoye alisema nafasi 45 za watendaji wa kijiji zilizotangazwa Agosti mwaka huu zimeshapata watu wa kuziziba.
CHANZO HABARI LEO 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa