Home » » NAIBU WAZIRI ,AKAGUA MAENDELEO YA MRADI WA MAJI CHALINZE

NAIBU WAZIRI ,AKAGUA MAENDELEO YA MRADI WA MAJI CHALINZE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Frank Mvungi-Maelezo
Serikali imesema kuwa inaridhishwa na hali ya utekelezaji wa mradi wa ukarabati na upanuzi wa mtambo wa maji Chalinze na ujenzi wa mfumo wa kusafirishia na kusambaza maji pamoja na matenki ya kuhifadhi maji utakaozalisha zaidi lita milioni tisa utakapokamilika.
Akizungumza wakati wa ziara yake ya kukagua mradi huo  utakaonufaisha wakazi zaidi ya laki tatu wa Jimbo la Chalinze na Wilaya ya Handeni Mkoa wa Tanga, Naibu Waziri wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji Mhandisi Ezekiel Kamwele amesema dhamira ya Serikali ya awamu ya Tano ni kuona wananchi wanapata huduma ya maji kwa wakati kupitia maradi huo unaotarajiwa kukamilika mwezi Oktoba mwaka huu.
“Mradi wa Lindi umekamilika na hapa lazima tuchukue hatua kama Lindi ili kutatua changamoto zinazoweza kukwamisha kukamilika kwa mradi kwa wakati  na kwa kuwa wametupa mpango kazi wao tunaamini kazi itakamilika kwa wakati na nitafuatilia kila hatua “ Alisisitiza Mhandisi Kamwele.
Akifafanua Mhandisi Kamwele amesema kuwa katika kila eneo la mradi alilokagua ikiwemo ulazaji wa mabomba, ujenzi wa matenki ya kusambazia maji ameridhishwa na kasi ya utendaji na kuipongeza Mamlaka ya Maji Safi na Maji taka Dar es Salaam (DAWASA) kwa usimamizi mzuri katika utekelezaji wa miradi ya maji wanayokabidhiwa.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Chalinze (CHALIWASA) Mhandisi Christer Mchomba amesema kukamilika kwa mradi huo kutasaidia kukuza shughuli za kiuchumi zikiwemo za viwanda kwa kuwa tayari wamepokea maombi ya Viwanda kadhaa kuunganishwa katika mtandao wa maji,viwanda hivyo ni Kiwanda cha shurubati (juisi), Kiwanda cha kutibu mbao, pamoja na Kiwanda cha kuzalisha vigae .
Aliongeza kuwa mradi huo pia utasidia kuinua shughuli za Kilimo na ufugaji hali itakayosaidia kukua kwa sekta ya Viwanda hali itakayochochea kukua kwa uchumi.
“Awamu ya Tatu  ya mradi huu inagharimu bilioni 84 hadi kukamilika kwake na huu ni mradi mkubwa utakaowanufaisha wananchi wengi” Alisisitiza Mhandisi Mchomba.
Katika kutekeleza mradi huo ulazaji wa mabomba  ya kusafirishia maji umefikia km 96.8 kati ya  km 115 na ujenzi wa ofisi umefikia asilimia 82.
Kwa upande wake Mwenyekiti mstaafu wa Kijiji cha Rupungwi Chalinze ambacho ni sehemu ya vijiji vinavyonufaika na mradi huo amesema wananchi wanapongeza Serikali kwa kuwaletea mradi huo utakaoinua shughuli za kiuchumi.
Mradi huu unatekelezwa kupitia mkopo kutoka India na mkataba wa ujenzi ulisainiwa tarehe 18 Mei, 2015 kati ya DAWASA na Kampuni ya Overseas Infrastracture Pvt Ltd ikishirikiana na PIL zote za India.



 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa