Home » » WANAKIJIJI WA KIJIJI CHA MAISHA PLUS WAMTEMBELEA KIJANA ALIYEPOTELEWA NA MAMA YAKE KATIKA MAZINGIRA YA KUTATANISHA

WANAKIJIJI WA KIJIJI CHA MAISHA PLUS WAMTEMBELEA KIJANA ALIYEPOTELEWA NA MAMA YAKE KATIKA MAZINGIRA YA KUTATANISHA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Kama kawaida asubuhi kulipopambanzuka wanakijiji cha Maisha Plus walifanya usafi katika maeneo yao na usafi wa kisima cha maji wanachotumia wanakijiji hao. Hii ni kuhakikisha wanaishi katika mazingira safi na salama na yenye kuvutia kijijini hapo. Kwa kuwa ni siku ya Jumapili wanakijiji hao hutumia siku hii kufanya ibada, kutembeleana na kujualiana hali. Baada ya kutoka kanisani wanakijiji walitumia fursa hii kwenda kumfariji mtoto aliyepotelewa na mama yake ambaye ametoweka kijijini hapo katika mazingira ya kutatanisha siku ya Jumamosi majira ya asubuhi na kumpatia kiasi cha shilingi elfu tano na mia moja ya pole. Hii inaashiria ushirikiano na umoja uliopo miongoni mwa wanakijiji cha Maisha Plus.


Wanakijiji walitawanyika na kuelekea katika kaya zao ambapo kila mwanakaya alielekea kwenye shamba lake na kujishughulisha na kilimo ili kukidhi mahitaji ya kaya zao. Ilipowadia nyakati za alasiri mtaalamu wa kilimo Bi. Janeth Maro kutoka shirika la Kilimo Endelevu Tanzania lenye makao yake makuu mjini Morogoro aliwatembelea wanakijiji cha Maisha Plus na kujionea namna wanavyojishughulisha na kilimo na wanavyokabiliana na wadudu wanaoshambulia mazao yao. Wanakijiji cha Maisha Plus walikuwa na shauku kubwa ya kutaka kujifunza zaidi kutoka kwa mtaalamu huyo kwa kuwa bustani zao za mboga mboga zinashambuliwa na wadudu waharibifu.

Mtaalamu wa kilimo Bi. Janeth aliwaeleza wanakijiji umuhimu wa kilimo hai ambacho kinatumia utaalamu wa hali ya juu kwa kuusoma udongo, kutumia mbinu za kurutubisha, kudhibiti magonjwa na wadudu na kuwa na mimea yenye afya na yenye nguvu ambayo haiwezi kushambuliwa na maradhi mbalimbali. Vile vile aliwasisitiza wanakijiji umuhimu wa kutumia mbinu ya kuhifadhi maji ardhini kwa kulima matuta yanayozuia maji ya mvua kwenda kasi na kuleta madhara kwenye mimea na hivyo kuifanya ardhi iwe na unyevu unyevu muda wote kama Mama Shujaa  Elinuru Moses Pallangyo alivyokuwa anaeleza na kuonyesha katika bustani yake iliyotumika kupata somo hilo.
Naye Mama Shujaa wa Chakula Grace G.D Maumbuka hakusita kutoa uzoefu wake katika kilimo hai anachojishughulisha nacho na kusema kuwa mara nyingi hupanda miti rafiki shambani ambayo majani yake huoza kiurahisi na kutunza unyevu unyevu ardhini. Vile vile alisisitiza kupanda mazao jamii ya kunde kwa kuwa inarutubisha udongo na kutolea mfano wa zao la njegere lilivyokuwa na faida kubwa kwa mkulima. Alisema zao la njegere halihitaji nguvu nyingi, si rahisi kushambuliwa na wadudu linapokuwa kavu na mimea yake haizalishi wadudu shambani na baadaye mimea hiyo hutumika kama mbolea.
Wanakijiji walifurahishwa sana na maelezo ya mtaalamu wa kilimo na kuuliza maswali mengi kwa kuwa walikuwa wana shauku kubwa ya kujua masuala mbalimbali hasa namna ya kukabiliana na wadudu waharibifu wanaoshambulia mazao yao hapo kijijini. Baada ya hapo wanakijiji walitawanyika na kuelekea katika kaya zao huku wengine wakijadiliana kuhusu somo hilo.

 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa