Home » » TUJIFUNZE KWENYE MVUA ZA UKANDA WA PWANI

TUJIFUNZE KWENYE MVUA ZA UKANDA WA PWANI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Kwa takriban siku tatu Watanzania hususan wa mikoa ya ukanda wenye mikoa ya Pwani, Dar es Salaam, Pwani na Morogoro walikuwa katika misukosuko kutokana na mvua kubwa iliyonyesha mfululizo katika maeneo hayo.
Mvua hiyo iliyobashiriwa mapema na Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) imesababisha maafa kwenye maisha ya watu, uharibifu wa mali na hata miundombinu ikiwamo barabara na madaraja. Tunatumia nafasi hii kuwapa pole wale wote ambao wameathiriwa na mvua hizo zilizosababisha pia hasara ambayo hadi sasa ni vigumu kuitathmini.
Pamoja na madhara kwa mtu mmoja mmoja au jamii kwa jumla ni jambo la kusikitisha kuona baadhi ya wananchi wakiwamo wanaoishi mabondeni au maeneo hatarishi wakiendelea kupuuza miito na hata tahadhari zinazotolewa, huku mamlaka zetu zikiwaachia waendelee kuishi huko.
Kwa upande wao, tunatumia nafasi huu kuendelea kuwasihi waondoke kwa hiari katika maeneo hayo kwani kulingana na TMA, bado mvua hizo zinaweza kunyesha na hivyo kuwasababishia maafa na hasara zaidi.
Pia tunatoa mkono wa pole kwa viongozi wetu, Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal, Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli na wengine wote walionusurika kwenye ajali ya helikopta iliyotokea mwishoni mwa wiki kwenye Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere wakati wakienda kukagua madhara yaliyotokana na mvua.
Hakuna shaka kwamba mvua hizo zitaigharimu Serikali kiasi kikubwa cha fedha katika kurudisha miundombinu hiyo katika hali yake ya kawaida. Tunaishauri serikali ifanye tafakuri ya kina kuhusu sababu za mafuriko hayo na namna ya kuyaepuka. Tunaamini zipo sababu za kibinadamu zilizochangia katika uharibifu huo wa miundombinu na ambazo zingeweza kuepukika.
Kwa mfano, kingo za baadhi ya barabara zimeathiriwa na ujenzi holela uliofanywa na wananchi huku mamlaka zetu zikiwatazama na hivyo kusababisha mmomonyoko ambao hatimaye husababisha barabara au madaraja kubomoka wakati wa mvua.
Aidha, wapo wananchi katika maeneo mengi ambao kwa makusudi wanaziba mifereji au mitaro ya maji ya mvua, kutupa taka kwenye madaraja, kiasi kwamba imekuwa rahisi kwa mvua kusomba na kuathiri miundombinu.
Tunaishauri Serikali, hasa Wakala wa Barabara (Tanroads) na mamlaka nyinginezo zikiwamo halmashauri zote, zichukue hatua za makusudi kuzuia kutokea tena kwa mambo kama hayo yanayoitia hasara nchi kwa kiasi kikubwa pia kupoteza maisha ya watu kama ambavyo imetokea kwenye mvua zilizonyesha siku chache zilizopita.
Tunashauri hatua zinazostahili zichukuliwe zikiwamo za kutunza mazingira kwenye miundombinu kama vile kuzuia ujenzi holela na uharibifu wa mazingira. Pia, tunaiomba Serikali itafute njia mbadala za kuepusha madhara yanayosababishwa na kufungwa kwa barabara kuu zinazoingia Dar es Salaam, Morogoro, Bagamoyo na Kilwa juzi na hivyo kusababisha usumbufu na hasara kiuchumi.
Njia hizo ni pamoja na kufufua reli ya kati na Tazara, kuhakikisha ujenzi wa barabara imara zitakaoifanya Dar es Salaam kuondokana na uwezekano wa kuwa kama kisiwa, kutekeleza mpango wa kujenga bandari za nchi kavu kuepusha athari za magari kwa barabara.
Kwa kufanya hivyo, tunaamini matatizo haya yatapungua kwa kiasi kikubwa.
reli hizi zitatumika kusafirisha shehena, abiria ukiwamo wakati wa dharura na hivyo kuokoa maisha, fedha ambazo zinapotea kwa kufungwa kwa miundombinu yetu.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa