Home » » JK:MAFURIKO HAYAEPUKIKI

JK:MAFURIKO HAYAEPUKIKI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

RAIS Jakaya Kikwete, jana ameshuhudia msururu mkubwa wa magari na maelfu ya wasafiri waliokwama katika eneo la Ruvu Darajani, mkoani Pwani, kutokana na kasi kubwa ya maji yanayopita juu ya daraja hilo.
Hali hiyo inatokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha katika mikoa mbalimbali nchini, kusababisha maafa kwa wananchi pamoja na uharibifu wa miundombinu hususan madaraja.
Miongoni mwa watu waliokwama eneo hilo ni Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, Bw. Job Ndugai aliyekuwa akitokea Dar es Salaam kwenda mkoani Dodoma.
Akizungumza katika eneo hilo, Rais Kikwete alisema mafuriko hayo hayaepukiki ambapo wajibu wa Serikali ni kuwasaidia waathirika, kwa taarifa alizonazo, 10 wamethibitika kupoteza maisha kutokana na mafuriko hayo.
"Mvua hizi zimekuwa na madhara makubwa kwani hata daraja la Bunju limebomoka na kukata mawasiliano kati ya Dar es Salaam na Bagamoyo.
"Kwa sasa Serikali inaangalia uwezekano wa kufungua Barabara ya Mlanzidi-Bagamoyo, kama kasi ya maji itapungua ili kupunguza msongamano wa magari," alisema.
Aliongeza kuwa, mafuriko hayo yamechangiwa na mvua ambazo zinaendelea kunyesha kwenye Milima ya Uluguru, mkoani Morogoro na kusabisha mito mingi kujaa maji.
Kutokana na hali hiyo, Rais Kikwete, ameliagiza Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Kambi ya Ruvu, kuhakikisha wasafiri waliokwama katika eneo hilo wanapata vyakula kwa bei nafuu.
Rais Kikwete alitoa agizo hilo baada ya kukuta sahani moja ya wali inauzwa sh. 4,000 na kuwataka wananchi wachukue tahadhari kwani mvua hizo bado zinaendelea kunyesha.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Bi. Mwantumu Mahiza, alisema hajawahi kuona mafuriko ya aina hiyo. Mvua hizo ambazo jana zimeingia siku ya tatu mfululizo, zimeendelea kuleta madhara kwa wakazi wa Jiji la Dar es Salaam, wengine wakikosa makazi.
Baadhi ya watu wamekuwa wakitafuta ndugu zao bila mafanikio kutokana na nyumba walizokuwa wakiishi kuzingirwa na maji.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa