Home » » Vikumburu hawana mawasiliano ya simu

Vikumburu hawana mawasiliano ya simu

WANANCHI wa Kijiji cha Vikumburu Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani wanaziomba kampuni za simu za mikononi kuwapelekea huduma ya mawasiliano.
Ombi hili lilitolewa mwishoni mwa wiki, katika mkutano wa kijiji ulioitishwa na Mwenyekiti wao Rashid Simba kujadili na kupitisha sheria za kulinda misitu.
Akichangia hoja Mjumbe wa Kamati ya Maliasili Said Mkwama alisema sheria walizopendekeza kwa kushirikiana na wenzao wa Halmashauri ya Kijiji ni nzuri lakini ulinzi wa kushtukiza utakuwa mgumu kutokana kukosa mawasiliano.
“Sheria tulizotunga ni nzuri na zitafanikisha kutunza na kuilinda misitu lakini tutashindwa kufanya ulinzi wa kushtukiza kwa kuwa hatuna mawasiliano ya mtandao wowote … hivyo tutaibiwa maliasili zetu,” alisema Mkwama.
Naye Seleman Dude alisema hivi sasa wanalazimisha mtandao wa Airtel kwa kupanda juu ya miti eneo moja porini ambalo waliliteua kwa ajili ya kupata mawasiliano.
Kutokana na hali hiyo ya kukosa mawasiliano, Dude alitoa rai kwa Mwenyekiti wa Kijiji kwa kushirikiana na viongozi wengine kufanya jitihada za kuwaombea mtandao katika kampuni mbalimbali za simu nchini ili nao waingie katika teknolojia.
Diwani wa Kata ya Vikumburu, Rashid Dihomba (CUF), alisema suala la kuwatafutia mtandao wa mawasiliano amelifanya kwa muda mrefu bila mafanikio hali inayomfanya atafsiriwe vibaya na wananchi wake.
“Inaniuma sana kuona wananchi hawanielewi pale ninapowaambia kwamba nafuatilia kampuni mbalimbali za simu ili zituletee mtandao wa mawasiliano, sitakata tamaa nitaendelea  hadi kieleweke,” alisema Dihomba
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa