Home » » RUBADA yawapa changamoto viongozi

RUBADA yawapa changamoto viongozi




WATENDAJI katika ngazi mbalimbali katika Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji, mkoani Pwani, wametakiwa kuendana na kasi ya kazi katika mfumo mpya wa usimamizi na ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo ili kufanikisha mpango wa Matokeo Makubwa Sasa. Changamoto hiyo ilitolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Uendelezaji Bonde la Mto Rufiji (RUBADA), Aloyce Masanja, mwishoni mwa wiki katika semina ya kuwajengea uwezo madiwani, watendaji mbalimbali katika ngazi za vijiji hadi tarafa juu ya mpango mpya wa usimamiaji na ufuatiliaji wa miradi ya maendeleo ya serikali wa Matokeo Makubwa Sasa.
“Lazima mchague maeneo ambayo yataleta matokeo makubwa, lakini vilevile nidhamu ya hali ya juu katika kufuatilia yale mliyoyapanga kutekeleza kwa kipindi fulani, bila hivyo hatuwezi kufika,” alisema Masanja.
Alisema ili nchi iweze kufikia katika malengo iliyojiwekea, ni lazima viongozi wawe na uthubutu wa kujiwekea malengo katika utekelezaji wa mipango yao katika maeneo yao na kushinda woga wa kushindwa.
Alisema katika mfumo mpya wa Matokeo Makubwa Sasa kila mtu atapimwa kulingana na kazi anayofanya na atakayeshindwa atawekwa pembeni na kuwaachia wale watakaoweza kumudu kazi husika.
Mkuu wa Wilaya ya Rufiji, Nurdin Babu, aliwataka watendaji hao kutoa ushirikiano kwa RUBADA, ili malengo yaliyowekwa na serikali ya mpango wa Kilimo Kwanza uweze kufanikiwa.
“Ndugu zangu, sisi sote ni mashahidi, hakuna asiyeona kazi kubwa inayofanywa na RUBADA katika kusimamia mpango wa kilimo katika eneo la Rufiji, tusipofanya hivyo tutabaki nyuma siku zote,” alisema Babu.
Aliongeza kuwa Wilaya ya Rufiji kwa sasa haina viwanda, na kwamba mkombozi pekee aliyebaki ni kujitahidi kuwekeza katika kilimo.

Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa