Home » » MAISHA YA KIBITI

MAISHA YA KIBITI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


HALI ya utulivu imerejea katika wilaya za Kibiti na Rufiji baada ya miaka miwili ya kutawaliwa na matukio ya mauaji.
Watu wasiopungua 40 wameuawa katika matukio tofauti yaliyofanywa na watu wasiojulikana na kusababisha wananchi kuwa na taharuki, kwa kuhofia maisha yao.

Watu waliofanya vitendo hivyo vya mauaji waliwalenga viongozi wa vyama vya kisiasa, serikali na askari wa Jeshi la Polisi, hali iliyosababisha shughuli za kiuchumi na kijamii kusimama pia.

Katika kilele cha mauaji ya kinyama mkoani Pwani, askari nane waliokuwa kwenye gari la polisi wakitoka kubadilishana lindo na wenzao waliuawa kwa risasi Aprili walipofika eneo la Mkengeni, kata ya Mjawa wilaya ya Kibiti Aprili 13, mwaka huu.

Waliouawa ni Mrakibu Msaidizi wa Polisi, Peter Kigugu, askari mwenye namba F.3451, Koplo Francis, F.6990 Konstebo Haruna, G. 3247 Konstebo Jackson, H.1872 Konstebo Zacharia, H.5503 Konstebo Siwale, H. 7629 Konstebo Maswi na H. 7680 Konstebo Ayoub.

Majambazi hao walipora bunduki saba ambazo ni SMG nne na Long Range tatu zikiwa na risasi zake. Hata hivyo, serikali kwa kutumia majeshi ya ulinzi na usalama inafanya operesheni maalum ya kupambana na wauaji hao, jambo ambalo limeleta ahueni kiasi kwa wakazi wa maeneo hayo, uchunguzi wa Nipashe umebaini.

Hivi karibuni nilifanya safari katika maeneo mbalimbali ya wilaya za Kibiti na Rufiji kujionea hali halisi ya maisha, hasa baada ya Inspekta Generali wa Polisi (IGP), Simon Sirro kutangaza kuuawa kwa majambazi 13 katika mapigano na askari wake Agosti 10.

Safari hiyo, iliyoanzia kituo cha mabasi yaendayo mikoa ya Kusini, kilichopo Mbagala Rangitatu, ilitumia saa 14 kuanzia saa 2:30 asubuhi.
Maeneo ambayo nilitembelea ni Jaribu, Bungu, Kibiti, Ikwiriri na Muhoro.

UKAGUZI WA KUTISHA
Ukaguzi ni jambo lililowekwa kipaumbele na vyombo vyote vya usalama, magari yote yakikaguliwa kwa ushirikiano baina ya polisi na askari wa Jeshi la Wananchi (JWTZ).
Kuanzia kituo cha Mkuranga, Jaribu, Bungu, Kibiti na Ikwiriri, abiria waliopanda kwenye mabasi yanayopita wilaya hizo walikaguliwa kuhakikisha wasafiri ni wale wenye vigezo. Vitu ambavyo vinaangaliwa kwa makini ni tiketi, vitambulisho vya kazi, uraia na cha mpigakura.

ULINZI KUIMARIKA
Nikiwa ndani ya gari, nagundua ulinzi umeimarishwa kila mahali, katika maeneo yote unaona magari ya polisi na jeshi yakipita.
Mfano, katika kituo cha Bungu nilishuhudia askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani wakifanya kazi zao huku wakilindwa vikali na askari wenye bunduki.
Juni 21, askari wawili wa Kikosi cha Usalama Barabarani wilayani Kibiti waliuawa kwa kupigwa risasi katika kijiji cha Msafiri, kata ya Bungu wakiwa kazini.
Mbali na kupigwa risasi, pia watu hao walichoma moto gari moja na pikipiki moja za askari hao kisha kutokomea kusikojulikana.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani wakati huo, Onesmo Lyanga alitaja majina ya 'trafiki' waliouawa kuwa ni Sajini Salum na Konstebo Masola.
Lakini wiki iliyopita, askari waliosheheni silaha nzito walisimama kila upande ambao trafiki amesimama.
Aidha, wakati katika maeneo mengi imezoeleka trafiki hufanya kazi zao kwa kutumia vibanda vilivyowekwa pembeni ya barabara, Kibiti na Rufiji ni tofauti.
Huko kuna magari maalumu ambayo hayaruhusu kupenye risasi, yanayotumika kama ofisi za askari hao.
Gari linaposimamishwa na kuonekana kuna matatizo, dereva anatakiwa kuingia katika gari hilo na huko ndipo ataandikiwa makosa yake na kupigwa faini.
Kwa madereva wanaondesha mabasi na malori yanayopita Barabara ya Kilwa, magari hayo ya trafiki si mageni kwao wameonyesha kuyazoea, kwa mujibu wa dereva wa basi nililosafiri nalo.
“Ni jambo la kawaida kwetu," anasema kondakta wa gari nililopanda, baada ya kumuuliza kama hawana hofu kuingia ndani ya gari lile ambalo limefanana na gari la kivita la daraya.
"Gari lile ni ofisi za trafiki." "Kule kuna huduma zote muhimu zinazotolewa na polisi.”

HAKUNA TOCHI
Jambo lingine nililoshuhudia ni pale magari yanayotumia barabara hiyo kukosa hofu ya kumulikwa tochi na askari wa Usalama Barabarani.
Madereva wa mabasi na magari mengine ni kama wamesahau suala la tochi za barabarani.
Kabla ya matukio hayo, madereva walikuwa wakilia kutokana na kulipa pesa nyingi za faini baada ya kumulikwa tochi na kuonekana kuendesha mwendo kasi kinyume na sheria.
Kuanzia Mkuranga katika kijiji cha Mwalusembe hadi kijiji cha Muhoro, Wilaya ya Rufiji, madereva wanaendesha magari yao kwa mwendo wanaoutaka. Kitendo hicho kinawashawishi baadhi ya madereva hao kujiongoza wenyewe, jambo ambalo linaongeza hatari ya kutokea ajali, hata hivyo.

BIASHARA ZADODA
Katika maeneo ambayo awali biashara zilishamiri kama Kibiti mjini, Jaribu, Bungu, Muhoro na Ikwiriri, sasa mambo mi magumu baada ya wafanyabiashara kulia njaa kwa kukosa wateja.
Wakizungumza kwa masharti ya kutotajwa majina yao, baadhi ya wafanyabiashara hao walisema licha ya hali kutulia, bado mzunguko wa biashara umekuwa mgumu.
Walisema tangu kuanza kwa mauaji na kisha serikali kuendesha operesheni ya kupambana na wauaji hao, shughuli za kibiashara si nzuri baada ya watu wengi kukimbia na kwenda mikoa ya jirani kwa kuhofia usalama wao.
“Unaona mwenyewe kama hapa Jaribu kulikuwa na maduka mengi, lakini idadi kubwa yamefungwa baada ya wamiliki wake kukimbilia jijini Dar es Salaam,” alisema mfanyabiashara mmoja.
Kauli ya mkazi huyo inaendana na hali halisi niliyoshuhudia katika eneo hilo. Maduka yalifungwa licha ya kuwa ni muda wa mchana na haikuonekana dalili ya kufunguliwa.
Wakazi wa eneo hilo walisema kwamba vijana wengi na watu ambao walipata hofu na mauaji hayo, waliamua kuondoka na kwenda sehemu zingine na kuacha nyumba zao tupu.
Hata hivyo wakazi hao walisema wanatarajia mambo yanaweza kubadilika baada ya serikali kutoa tamko la kutaka watu kurejea kwenye maeneo yao kwa kuwa hali ya amani imerejea.
“Baada ya serikali kusema hali ni shwari, naamini watu wataanza kurejea na kurudisha mfumo mzima wa maisha uwe kama zamani,” alisema mkazi mmoja wa Bungu.

HASARA SHAMBANI
Shughuli za kilimo cha mazao ya chakula na biashara zilisimama baada ya wakulima kutelekeza mashamba yao kutokana na hali duni ya usalama.
Mashamba ya mihogo, ambayo inategemewa kwa ajili ya chakula na biashara mengi yametelekezwa na kugeuka mapori.
Mkulima mmoja wa kijiji cha Mtawanya alisema wameshindwa kwenda kupalilia mashamba yao kwa kuhofia usalama wao.
“Mimi nina heka tano ya mihogo, lakini nimeshindwa kuipalilia baada ya kuogopa kwenda shambani.
Nimepata hasara na sijui nitakula nini kwani zao hili nalitegemea kwa kuniingizia kipato,” alisema mkulima huyo.
Kilio kama hicho kimewakumba wakulima wa zao la ufuta katika vijiji vya Muhoro na Ikwiriri, ambao walisema wameshindwa kulima mwaka huu licha ya kutumia fedha nyingi kuandaa mashamba na kununua dawa.

WENYE BAA WAPUMUA
Kwa upande wa biashara za vinywaji na burudani, wao kidogo wameonekana kupumua, baada ya muda wa kufanya biashara zao kuongezwa mpaka saa 6:00 usiku.
Mmiliki wa baa moja mjini Kibiti, aliliambia gazeti hili kwamba huko nyuma walikuwa wakisitisha biashara zao saa 3:00 usiku.
“Kwetu sisi tunaouza vinywaji kidogo tumepata nafuu, serikali imetutaka tufunge shughuli zetu saa sita usiku. Kinachotuumiza kwa sasa ni ukosefu wa wateja tu,” alisema mmliki hiyo.

BODABODA BADO KIBANO
Madereva wa pikipiki maarufu kama ‘bodaboda’ bado wanaendelea na kibano cha katazo la kutumia vyombo vyao inapofika saa 12:00 jioni.
Baadhi ya madereva walisema hakuna kilichobadilika tangu serikali ilipoanza kulegeza baadhi ya amri. “Kuna baadhi ya biashara zimelegezwa masharti, lakini sisi bodaboda bado tunaendelea kufanya biashara hadi muda uliowekwa na serikali,” alisema dereva mmoja katika kituo cha mabasi cha Ikwiriri.
Hata hivyo, katika vijiji vilivyo ndani njia rahisi ya usafiri ni bodaboda. Endapo mtu atashuka kituo cha basi baada ya saa 12:00 jioni humlazimu kulala au kutembea kwa miguu iwapo ni jasiri.
“Tunapata wakati mgumu pale anapotokea mteja anayekwenda vijiji vilivyo mbali na hapa, hatuwezi kuwasafirisha kwa kuhofia kukamatwa,” alisema kijana mwingine.
Pamoja na hali hiyo, vijana hao walionekana kuwachangamkia kwa bashasha abiria kana kwamba hakuna jambo lolote linaloendelea.

KUFULI OFISI WATENDAJI
Siku ambayo nilifika eneo hilo niliona baadhi ya ofisi za watendaji wa vijiji zikiwa bado hazijafunguliwa na nyingine zikifanya kazi, lakini kwa mwendo wa kusuasua.
Katika ofisi ya kijiji cha Chumbi, nilishuhudia ofisi zikiwa tupu, huku mtendaji wake na mwenyekiti nikielezwa wameshindwa kuingia ofisini muda mrefu.
Baadhi ya wakazi wa kijiji hicho, walisema wanapohitaji huduma inawabidi kwenda Utete au Muhoro.
“Hakuna huduma iliyoanza kutolewa, labda kutokana na serikali kutangaza (viongozi) warudi pengine tutawaona wakifanya kazi,” alisema mkazi mmoja wa kijiji hicho.
Hali hiyo ni tofauti katika kijiji cha Muhoro, kwani watendaji wake wamekuwa wakifungua ofisi zao na kutoa huduma kila siku.
Hata hivyo ofisi hizo zinafungwa kabla ya saa kumi jioni.
Chanzo:Nipashe

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa