Home » » Noah, ‘vipanya’ kutopewa leseni mpya njia kuu Pwani

Noah, ‘vipanya’ kutopewa leseni mpya njia kuu Pwani

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
  

John Gagarini, Kibaha
KUTOKANA na kukithiri kwa ajali za mabasi madogo aina ya Noah, Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra) mkoani Pwani imesitisha utoaji leseni mpya kwa magari hayo yanayojulikana zaidi kwa jina mchomoko na Hiace katika barabara kuu zote, ikiwamo ya Morogoro.
Noah pamoja na pikipiki zimeelezwa kusababisha vifo vya watu 102 huku 246 wakijeruhiwa katika kipindi cha kuanzia 2015 hadi Machi 2016.
Akizungumza na wanahabari mjini Kibaha, Ofisa Mfawidhi wa Sumatra mkoa wa Pwani, Nashon Iroga, alisema kwa mujibu wa waraka walioupata kutoka makao makuu, magari hayo yote madogo ya abiria yanayokwenda masafa marefu kupitia barabara kuu hayatapewa leseni ya kubeba abiria.
“Barabara kuu kuna vyombo vikubwa vya usafiri hivyo hayataruhusiwa kupata leseni mpya, badala yake yaliyokwisha pata leseni yataendelea hadi hapo mwongozo mwingine utakapo tolewa,” alisema Iroga.
Alisema, agizo hilo limetolewa baada ya ongezeko kubwa la magari madogo ya kubeba abiria hasa magari aina ya Noah, kufanya safari ndefu huku baadhi yakiwa yamebeba abiria na mizigo bila kuangalia usalama wa abiria na matokeo yake ni kusababisha ajali za mara kwa mara na msongamano katika barabara kuu.
“Ukiangalia kwa hali ya kawaida magari aina ya Noah yanabeba abiria wachache lakini ili wapate faida inabidi watoze viwango vikubwa vya nauli, kubeba abiria kuliko uwezo wake na kwenda mwendo kasi ili wafanye safari nyingi na kupata faida, matokeo yake wanahatarisha usalama wa maisha ya abiria,” alisema Iroga.
Aidha, alisema magari hayo madogo yakiwamo Noah na Hiace yanayobeba abiria yatapewa lesseni mpya za kufanya biashara kutumia ruti za barabara za ndani na sio barabara kuu.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa