Home » » UMASKINI WAITESA MAFIA

UMASKINI WAITESA MAFIA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mafia ni moja ya wilaya zilizoko mkoani wa Pwani. Shughuli nyingi za kiuchumi katika wilaya hiyo zinategemea uvuvi, kilimo cha nazi pamoja na utalii. Hata hivyo shughuli hizo hazijaweza kuondoa hali duni ya maisha ya watu wake.
Mafia ina wakazi wapatao 46,000, kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012.Wakazi wa wilaya hiyo walio wengi wanakula mlo mmoja kwa siku, hii inatokana na wengi wao kutegemea uvuvi wa samaki pekee, ambao kwa bahati sasa ni vigumu kuwavua kutokana na kuwepo kwa sheria mbalimbali zinazowazuia wageni kuvua wanavyotaka kama ilivyokuwa zamani.
Baadhi ya wakazi wanasema zamani kulikuwa hakuna ulazima wa kuomba kibali, lakini sasa mvuvi anapaswa kuomba kibali, huku pia kukiwa na sheria kali za kumwongoza mvuvi wapi pa kuvua au wapi pa kutovua.
Kwa sasa wilaya hiyo ina kiwanda kimoja cha minofu ya samaki. Wakati kinajengwa, wananchi wengi wanamini kwamba wangepata ajira, hata hivyo ukweli ni tofauti, kiwanda kina uwezo mdogo sana wa kutoa ajira.
Mkurugenzi wa Wilaya ya Mafia, Fransic Namaumbo anasema kiwanda hicho cha Tanpesca kinachangia Sh8.4 milioni kwa mwezi katika wilaya hiyo kwa mwaka kama kodi.
Shughuli za uvuvi
Na maumbo anasema uvuvi wa samaki kwa ujumla unachangia pato kwa wilaya hiyo Sh129 milioni.
Kulingana na kiongozi huyo wastani wa kipato cha mkazi wa Mafia kwa siku ni Sh1,350, kiasi ambacho baadhi ya wananchi wanapingana nacho wakisema kuwa kwa namna wanavyoona, wananchi wengi wana kipato kidogo zaidi ya hicho.
Wananchi wengi wanalalamika kwamba viongozi wa wilaya hiyo hawasimamii vizuri rasilimali zilizopo. Wanadai kuwa wanashindwa kuwaongoza vema wananchi kuelekea kwenye mafanikio.
Miundombinu mingi ni duni, huduma nyingi za afya si bora, kiasi kwamba wilaya nzima inategemea hospitali moja tu kubwa ambayo nayo imekuwa ikilalamikiwa kutokuwa na vifaa vya kutosha katika kuhudumia wananchi.
Huduma za afya, elimu, maji safi na salama na barabara ni mojawapo ya kero kubwa zilizoko katika Wilaya ya Mafia, huku wenye madaraka wakilaumiwa kutoa ahadi nyingi zaidi kuliko vitendo.
Baadhi ya wafanyakazi wanaopangwa kufanya kazi Mafia kutoka mikoa mingine, hukimbia, kutokana na miundo mbinumingi kuwa duni.
Wilaya hiyo ina umaarufu wa kilimo cha aina mbalimbali kama cha minazi, ambayo huingiza fedha nyingi kwa serikali ya wilaya. Kuna wakazi wengi ambao maisha yao yanategemea kuuza nazi.
Ni kutokana na kuuza nazi, baadhi ya watu wamekuwa wakifungua miradi ya maendeleo licha ya kwamba mingi ni midogo.
Kulingana na taarifa ya wilaya hiyo, hekta 26,000 za ardhi zinatumiwa kwa kilimo cha minazi, mingi ilipandwa muda mrefu sana. Baadhi ya minazi hiyo haizai na kilimo chake siyo cha kisasa.
Kwa sasa Mafia kuna minazi 52,000 inayozalisha tani 32 hadi 34,000 za nazi kwa mwaka na kila nazi moja huuzwa Sh300, hii ikiwa na maana kuwa kwa biashara ya nazi pekee huingiza wastani wa Sh4.8bilioni kwa mwaka.
Hata hivyo, baadhi ya wananchi wanasema biashara hiyo imekuwa haina msaada mkubwa kwa wakazi wa kawaida kwa vile walio wengi huuza nazi moja au chache. Wenye kupata faida kubwa ni wale wanaonunua nazi nyingi kwa wananchi na kwenda kuziuza kwa jumla.
Wafanyabiashara hununua kwa bei waitakayo, hata chini ya Sh300, licha ya ukweli kwamba walio wengi huwa wanakwenda kuuza hadi Sh500 kwa nazi.
Halmashauri hutoza gunia moja la nazi kwa ushuru wa Sh1000; gunia huwa na wastani wa nazi 200 hadi 300. Licha ya kuwa na wingi wa nazi. Mafia hakuna kiwanda cha kutengeneza mafuta ya nazi wala tui linalotokana na nazi.
Nje ya zao la nazi, hekta 240,200 hutumika kwa ajili ya kilimo cha mazao ya mpunga, mahindi, mihogo, ndizi mazao ya kunde viazi vitamu, nyanya, mtama, michungwa, miembe, korosho na mboga.
Kwenye ushuru wa mazao mbalimbali ya kilimo mwaka 2011/2012 halmashauri ilikusanya Sh25 milioni. Mwaka 2012/2013 ilikusanya Sh38 milioni ikiwa ni sawa na asilimia 126 kutoka kwenye lengo la kukusanya Sh30milioni.
Mwaka huu makisio ni kukusanya Sh30 milioni na hadi kufikia Februari walikuwa wamepata Sh18 milioni, sawa na asilimia 62 ya lengo.
Aidha kupitia leseni za uvuvi halmashauri katika mwaka 2011/2012 ilipata Sh50 milioni, japo makisio yalikuwa ni kupata Sh42 milioni.
Fedha hizo zimetumika kujenga barabara, kujenga zahanati nne ambazo mpaka sasa zipo katika hatua za mwisho na kuwekwa vifaa na wahudumu, pamoja kununua dawa katika hospitali ya wilaya.
Hata hivyo, wananchi wengi wanaomba Serikali iwaangalie kwani wana hali duni mno kiuchumi, licha ya halmashauri kutangaza kukusanya fedha nyingi.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa