Babu-akiwakaribisha wageni wa WLAC waliofika Kijijini kwa ajili ya kutoa Semina
Baadhi ya wanakijiji wakiwa wanasikiliza kwa makini katika Semina hiyo
Malkia wa kijiji cha Maisha Plus Mary Mwanga na washiriki wengine wakifuatilia mjadala
Bango la unaweza kuwa mzazi asiyekubali binti yake aolewe katika umri mdogo likiwa katika moja ya nyumba ya Kijiji cha Maisha Plus.
Kisa cha kwanza kikisomwa kwa makini
Kisa kikiendelea kusomwa kwa makini
Mmoja ya washiriki wa Maisha Plus/ Mama Shujaa wa chakula wa Chakula akigawa vijarida
Faudhia Yasin kutoka WLAC akielezea kwa kina masuala mbalimbali kuhusu Wanawake kuwa wasimamizi wa Mirathi
Aliyesimama Mbele ni Juvenile Rwegasira akizungumzia jambo muhimu na kutoa mafunzo kuhusiana na Ndoa Halali
Baadhi ya Washiriki wa Maisha Plus/Mama Shujaa wa chakula wakiwa wameanika baadhi nguo zao
MamaShujaa Grace Mahumbuka akiwasilisha mada muhimu wakati wa mkutano huo Kushoto ni BakariKhalid kuliani Said Kawawa
Wanakijiji wakiwa katika makundi wakijadili mambo kadha wa kadha
*************
Ikiwa ni
siku ya tatu toka Mama Shujaa wa chakula waingie kijijini Maisha Plus na siku
ya 37 toka mashindano hayo yaanze rasmi, jopo la Wanasheria kutoka shirika
lisilo la kiserikali la WLAC juzi lilitua kijijini hapo kwa ajili ya kutoa
mafunzo mbalimbali ya kisheria kwa wanakijiji hao.
Wanasheria
hao ambao ni Faudhia Yasin, Sarah Mambea na Juvenile Rwegasira walianza kwa
kuwagawa washiriki katika makundi matatu na kisha kuwataka wajadili visa
walivyopewa.
Visa hivi
vitatu vililenga kupata ufahamu wa wanakijiji juu ya mambo yanayohusiana na Mjane
na urithi, sheria ya ndoa na talaka pamoja na ukatili dhidi ya wanawake.
Makundi yawasilisha visa
Kundi la kwanza
liliwakilishwa na washiriki Mbonimpaye Nkoronko kutoka Mtwara, Boniphace Meng’anyi
kutoka Dar es salaam na Ngabonziza Daniel kutoka nchini Rwanda. Vijana hawa
katika kisa chao waligundua kwamba mtu akishakuwa katika ndoa kwa muda wa miaka
mitatu tayari anakua mwanandoa halali.
Kundi hili
lilitoa mapendekezo ya kutolewa kwa elimu juu ya masuala ya ndoa kabla ya watu
kuingia katika ndoa na uwepo wa sheria za kuondoa ukatili na kuleta usawa
katika jamii zetu. Boniphace alisisitiza kwamba uwepo wa sheria madhubuti ndio
mkombozi pekee wa wanyonge kwani bila hivyo watu walio matajiri wanapendelewa.
Mshiriki
Ally Thabit kutoka Mwanza alichaguliwa kutoa mrejesho wa kundi namba mbili
ambao kisa mkasa chao kilimuhusu Bwana Musa ambaye alifungua akaunti tatu za
siri na pia kujenga hoteli kisiri bila mkewe kufahamu, kisa hicho mwishoni
kinaonyesha Bwana Musa alifariki ghafla na hivyo kuleta msuguano mkali sana
katika familia yake kuhusu mgawanyo wa mali.
Huku
akijibu maswali ya mirathi yaliyojitokeza katika kisha hicho Ally anataja,
miongoni mwa hasara nyingine, kwamba kwanza haki ya urithi imepotea, pili usiri
wa baba umekuwa kikwazo katika familia kupata haki ya msingi lakini tatu kwamba
huenda wakati Bwana Musa anafariki kulikuwa na pesa nyingi katika akaunti yake
benki ambazo zingeisaidia familia yake ambayo kwa mujibu wa kisa hicho hivi
sasa familia hiyo inakumbwa na janga kali la umaskini.
Katika
kuelezea umuhimu wa wosia; Ally anaendelea kusema kwamba wosia huondoa utata
inapotokea kifo na vilevile wosia huondoa chuki na fitna baina ya ndugu na
jamaa.
Mwanamke anaweza kuwa msimamizi wa mirathi
Naye
Faudhia Yassin ambaye ni mratibu wa kampeni ya TUNAWEZA (www.facebook.com/TunawezaZuia)
kutoka WLAC aliwaeleza wanakijiji kwamba Mwanamke amekuwa akitengwa sana katika
ugawaji mali hivyo ni muhimu jamii kutambua kwamba hata wanawake waliofiwa na
waume zao wanaweza kuwa wasimamizi halali wa mirathi.
Faudhia
alisema ikitokea baba amefariki, familia ichukue cheti cha kifo na kukipeleka
mahakamani kuomba mahakama imuidhinishe waliyempendekeza kuwa msimamizi wa
mirathi.
Ndoa halali ni ipi?
Kundi la
tatu linawakilishwa na Mama Shujaa wa chakula Grace G.D. Mahumbuka kutoka
Kagera pamoja na vijana wa Maisha Plus ambao ni Bakari Khalid kutoka Shinyanga
na Said Kawawa kutoka nchini Uganda.
Kundi hili
linagundua kwamba mtoto wa kike hathaminiki kama ilivyo kwa mtoto wa kiume,
lakini elimu pia ya uelewa juu ya mambo ya haki ni duni. Sehemu ya kisa hicho
inawataja watu wawili wa jinsia tofauti walioishi pamoja kwa kipindi cha miaka
12 bila kuwa na ndoa hata ya kimila.
Aidha kundi
hili linapendekeza sheria ya ndoa ya Tanzania iboreshwe na kwamba ifahamike
kuwa mtoto wa kike ana haki ya kurithi sehemu ya mali ya wazazi wake sawa sawa
na ilivyo kwa mtoto wa kiume.
Wanapendekeza
kwamba inapotokea tatizo katika ngazi ya familia baina ya mke na mme basi
aliyetendewa ukatili ajaribu kusuruhisha katika ngazi ya familia ikishindana
basi aende katika ustawi wa jamii, baraza la kata, ofisi za ushauri wa kisheria
za mashirika ya kiserikali na yasiyo ya kiserikali kama itashindikana kote huko
basi mwisho achukue hatua za kisheria za kimahakama.
Akifafanua
kuhusu hoja hii, Mwanasheria Juvenile Rwegasira kutoka WLAC alisema kwamba watu
wawili wa jinsia tofauti wakiishi pamoja kwa kipindi cha miaka miwili
mfululizo na jamii ikafahamu kwamba hawa
ni mme na mke, hiyo kisheria inaitwa dhana ya ndoa.
Mwanasheria
Rwegasira alisisitiza kwamba ni lazima iwe miaka miwili mfululizo na sio ile ya
kuja miezi miwili na kuondoka na kuja tena na kuondoka.
Hata hivyo,
Bw. Rwegasira alitoa angalizo kwamba ndoa hii ni rahisi sana kukanushika hivyo
akasisitiza umuhimu wa kuhitaji tamko la Mahakama kuidhinisha dhana ya ndoa.
Akiendelea Bw. Rwegasira alisema kwamba ndoa hii ni ya kienyeji mno na haina
cheti hivyo ikitokea mmoja amefariki inaleta shida sana kwenye ugawaji wa mali.
Pata msaada wa kisheria BURE
WLAC ni
kituo cha msaada wa kisheria kwa wanawake. Kwa wenye matatizo ya Mirathi, Ndoa,
Ardhi, Elimu, Ajira, Matunzo ya Watoto na Mengineyo wapige simu BURE kwenda
namba 0800780100.
Endelea kufuatilia mashindano ya Maisha
Plus/Mama Shujaa wa Chakula kila siku za Jumapili – Alhamisi saa 4 usiku na
Ijumaa na Jumamosi saa 3 usiku kupitia TBC1.
Taarifa zote pia zinawekwa www.facebook.com/MamaShujaa na www.facebook.com/MaishaPlus
Wekeza kwa wakulima wadogo wanawake. INALIPA.
Maisha Plus. REKEBISHA.
0 comments:
Post a Comment