Home » » Wapatiwa mafunzo kutatua migogoro

Wapatiwa mafunzo kutatua migogoro

SERIKALI wilayani Mkuranga, Pwani, imeombwa kutoa elimu ya sehemu sahihi ya kufikisha migogoro ya ardhi na namna ya kuitatua, ili kupunguza wimbi la migogoro hiyo.
Ombi hilo lilitolewa mwishoni mwa wiki na baadhi ya wakazi wa Mkuranga baada ya kupatiwa mafunzo ya sheria namba saba ya mabaraza ya kata ya mwaka 1985 na Asasi isiyo ya Kiserikali ya Ushirikiano wa Vijana wa Mwandege (USHIVIMWA).
Akizungumza baada ya mafunzo hayo, mmoja wa washiriki hao, Shwaari Maneno, alisema wananchi wanatakiwa kupatiwa elimu hiyo ili waweze kujua sehemu sahihi ya kupeleka migogoro yao.
Veronika Mloka mjumbe wa baraza la kata ya Kiparang’anda alisema migogoro mikubwa katika maeneo yao ni ya ardhi ambayo wakati mwingine inatishia amani kwa walengwa.
Mloka aliiomba serikali kufikisha elimu kwa wananchi na viongozi wa mabaraza, ili migogoro hiyo imalizike katika ngazi ya kata badala ya hali ilivyo sasa ya kuifikisha polisi na kurudi tena kata hali inayochangia kutumia muda mwingi.
“Kabla ya kushiriki mafunzo haya sikujua namna ya kuendesha mabaraza wala kuwaelekeza wananchi waanzie wapi wanapokua na kesi kama hii sasa nitatoa elimu hii kila utakapofanyika mkutano ili wananchi waelewe,” alisema.
Katibu Mtendaji wa Asasi hiyo, Nuri Kiswamba, alisema wamefikia hatua ya kutoa mafunzo hayo baada ya kuona ongezeko kubwa la migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa