Home » » Pwani wahimizwa kulima ufuta

Pwani wahimizwa kulima ufuta

MKUU wa Mkoa wa Pwani, Mwantumu Mahiza, ametoa wito kwa wenyeviti wa halmashauri zote za mkoa huo kusisitiza kilimo cha ufuta ambacho kitakuwa mbadala wa zao la korosho linalosuasua kwa sasa.
Mahiza alitoa wito huo mwishoni mwa wiki alipozungumza na wadau mbalimbali wa kamati ya ushauri ya mkoa huo kwenye kikao chake kilichofanyika mjini Kibaha.
Alisema kwa sasa zao la korosho linasuasua, hivyo ni vema viongozi wakasisitiza kilimo cha ufuta kitakachowakomboa wananchi wengi hasa katika suala la maendeleo.
“Wenyeviti wa halmashauri himizeni kilimo cha ufuta katika maeneo yenu, wakazanieni wananchi wenu katika suala la kilimo kitasaidia kuwawezesha kulipa ada za watoto na kufanya mambo mengine ya kimaendeleo,” alisema.
Aidha, alisema endapo wananchi hao watajikita katika kilimo cha zao hilo kitawasaidia pia kulipa gharama za mfuko wa bima ya afya na kuongeza idadi ya wananchi wanaojiunga na mfuko huo.
“Mtu akishindwa kulima ufuta basi afuge kuku; wekeni sheria za kujiunga na mfuko wa bima ya afya, ili kila mwananchi aweze kujiunga. Natambua hali ya uchumi ya wananchi wangu tusipowakazania katika kilimo hakutakuwa na maendeleo,” alisema.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa