Home » » Watumishi wa Mahakama watakiwa kufuata maadili

Watumishi wa Mahakama watakiwa kufuata maadili

JIBU LA SWALI LA MBUNGE Kibaha vijijini



SERIKALI imewataka watumishi wa Mahakama nchini ambao hawataki kufuata sheria, kanuni na maadili ya kazi yao kuondoka mara moja kazini.
Kauli hiyo ilitolewa bungeni jana na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angellah Kairuki, alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Kibaha Mjini, Silvester Koka (CCM), aliyetaka kujua mkakati wa serikali katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili watendaji wa mahakama, ikiwamo ukosefu wa nyumba, sare na masilahi duni yanayochangia kupokea rushwa.
Katika swali lake la msingi, mbunge huyo alitaka kujua mpango wa serikali katika kujenga jengo jipya la Mahakama ya Mwanzo kwenye Halmashauri ya Mji wa Kibaha, ili iweze kutoa huduma zake sawasawa.
Katika swali la nyongeza, Mbunge wa Karatu, Israel Naste (CHADEMA), alitaka kujua nini kimetokea katika maendeleo ya ujenzi wa Mahakama ya Wilaya ya Karatu ambao ulikuwa ukienda kwa kasi na kwa sasa umesimama.
Akijibu maswali hayo, naibu waziri huyo alisema tayari wameshawasiliana na wasajili wa wilaya wa Mahakama kupata orodha ya watumishi wanaohitaji sare na kuongeza kuwa changamoto ya nyumba na masilahi vinashughulikiwa.
Alisema azima ya serikali ni kuona watumishi wote wa Mahakama wanatekeleza wajibu wao kama walivyoapa.
Pamoja na hayo, alikiri jengo la Mahakama ya Mwanzo Kibaha Maili Moja ni bovu na tayari serikali imeshatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo.
Alisema mpaka sasa taratibu za kumpata mshauri mwelekezi kwa ajili ya usimamizi wa ujenzi wa jengo hilo zinakamilishwa ili kuwezesha ujenzi huo kuanza mara moja.
“Ni mpango wa serikali kujenga majengo mapya katika mahakama zote ambazo majengo yake ni mabovu na chakavu,” alisema naibu waziri huyo na kuongeza kuwa kutokana na ufinyu wa bajeti wataendelea kujenga majengo ya mahakama kadiri hali ya bajeti ya fedha itakavyoruhusu

CHANZO;TANZANIA DAIMA

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa