Home » » Utondwe, mji wa kale uliosahaulika Bagamoyo

Utondwe, mji wa kale uliosahaulika Bagamoyo

Niliposoma Kitabu cha Sir Francis R. Burton, Zanzibar, alichokiandika mwaka 1857, anasema aliwahi kutembelea Saadani, mji wa kale alikokuwa anakaa Sultan Bwana Heri ambaye alishirikiana na Bushiri bin Salim al-Harith.
Anasema aliambiwa habari za kuwapo kwa mji wa kale uliopo Kusini mwa eneo hilo, Utondwe. Burton anasema aliwahi kusoma kuhusu mji huo katika maandishi ya al-Masoud, msafiri maarufu sana enzi za karne ya kumi
Al-Masoud alitembelea maeneo hayo karne ya kumi. Na Wareno walianza kuja Pwani karne ya kumi na nne na kumi na tano. Basi Utondwe ni miongoni mwa miji ya kale sana katika historia ya pwani yetu.
Baada ya kusoma kitabu hicho nilifunga safari hadi Bagamoyo, nilipowauliza watu wanaofanya kazi Idara ya Mambo ya Kale, walisema hawajui na hawajawahi kusikia habari za mji huo. Mmoja wa watu alisema alishawahi kusikia habari za mji huo wa kale, lakini hajawahi kufika kwenye mji huo ingawa anasema alielekezwa ulipo.
Wazee wengi wa umri wa kati ya miaka 50 na 60, walisema hawajawahi kuusikia. Nilipofanya utafiti kwenye mtandao wa intaneti nikaona picha za maandishi ya Kiislamu (Islamic Inscriptions), ambayo yaliandikwa kwenye makaburi ya Utondwe. Wazungu walishafika na kufanyia utafiti, na kuchukua vibao hivyo vya maandishi kwenye makaburi.
Nilifunga safari kwa boda boda na kutembelea mji huo ambao uko kilomita 50. Wenyeji wa eneo la Kitame wanalijua eneo hilo, lakini hawajui kama paliwahi kuwa na mji. Kuna mashamba ya chuo na mto wa maji chumvi, mkondo wa bahari kama alivyoeleza Francis Burton. Burton alieleza kuwa eneo hilo lilikuwa likizalisha chumvi.
Nilipokuwa naangalia kwenye vichaka na vichuguu niliona dalili za kuwa watu waliwahi kuishi hapo. Pia nilitembelea msitu na baadaye nilitokea kwenye msikiti ambao sasa umebaki kuta tu na nguzo za ndani. Paa hakuna, hakuna makazi ila makaburi mawili jirani, na moja umbali wa mita kama ishirini, na mengine yamezolewa na mto unaopanuka. Hii ni hifadhi ya historia, lakini hakuna anayeujua mji huu wa kale wa Utondwe, wilayani Bagamoyo.

CHANZO;MWANANCHI

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa