Home » » Mapunda: UVCCM ni ya vijana wote

Mapunda: UVCCM ni ya vijana wote



JUMUIYA ya Umoja wa Vijana (UVCCM) imesema kuwa taasisi hiyo ni ya vijana wote bila kujali chama kutokana na changamoto za vijana hao kutatuliwa na serikali yenyewe kwa kuthamini mchango wao. Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa UVCCM taifa, Sixtus Mapunda, wakati akizungumza na wananchi wa mji wa Kibaha kwenye viwanja vya Mwendapole ambapo alisema kuwa katika kutafuta ufumbuzi wa changamoto za vijana serikali haiangalii itikadi ya chama.
Mapunda alisema UVCCM ina mpango wa kuainisha vipaumbele vya vijana kuwa pamoja na kuwatambua na majukumu yao ili wanapoanza utekelezaji watambue eneo mahususi la kuanzia kuhakikisha kila kijana anajishughulisha badala ya kuisubiri serikali kuwaajiri.
Akizungumza katika mkutano huo baada ya kusimikwa kuwa kamanda wa vijana, mbunge wa Kibaha Mjini, Silvestry Koka, alisema ili kuwezesha kila kijana anajiajiri mwenyewe, kuna mpango mkakati aliouandaa kwa kugawa pikipiki kwenye kata 11 za mji huo.
Koka alisema pikipiki hizo zitagawiwa kwa uongozi wa madereva pikipiki ulioko kwenye kata ili waitumie kwa pamoja na baadaye kununua nyingine ili kuhakikisha kila kijana anamiliki pikipiki yake mwenyewe.
Akizungumzia suala la afya, alisema hivi karibuni anatarajia kukabidhi vifaa tiba vyenye thamani ya sh milioni 25 katika awamu ya kwanza na awamu ya pili vifaa tiba vitasambazwa katika hospitali na vituo vya afya vilivyoko katika mji huo vikiwa na thamani ya sh milioni 700.
Katika mkutano huo wanachama wa CCM waliaswa kuwa na msimamo katika chama chao na kuacha tabia ya kuyumbishwa na viongozi wa vyama vya upinzani ambao alidai wengi hawana nia njema na wananchi. 

Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa