Home » » Rais Kikwete kufanya ziara ya siku 6 Mkoani Pwani

Rais Kikwete kufanya ziara ya siku 6 Mkoani Pwani

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Jakaya Kikwete anatarajiwa kuanza ziara ya siku sita mkoani Pwani wiki hii ambapo pamoja na mambo mbalimbali atakayofanya pia atakabidhi gari moja la wagonjwa na boti mbili aina ya ambulance boats kwa ajili ya kuwasaidia wagonjwa wa visiwani katika Delta za mto Rufiji na kuzindua mradi wa uwanja wa ndege wa Mafia na gati.

Katika ziara hiyo inayotarajiwa kuanza wilayani Mafia Oktoba 3 na kuendelea wilaya zingine hadi Oktoba 9,Dkt Kikwete pia atazindua na kuweka mawe ya msingi ya shughuli mbalimbali za kimaendeleo katika sekta ya Elimu, Afya Viwanda na shughuli za vijana ambao wamejiajiri baada ya kupata mafunzo kwenye kambi za maarifa.

Mkuu wa mkoa wa Pwani,Hajat Mwantumu Mahiza amebainisha kuwa Rais ameamua kuanza ziara yake hiyo Wilayani Mafia wilaya ambao mkoani humo ipo kisiwani na imekuwa ni ngumu watu wengi kuitembelea mara kwa mara kutokana na jiografia yake kuwa ngumu na usafiri wake ni wa shida kufuatia meli kushidwa kufika baada ya gati kuharibika.

Pia katika wilaya zingine Dkt Kikwete ataweka mawe ya msingi na kuzindua miradi ya maendeleo kwenye sekta za Elimu, Afya, Viwanda, Uchukuzi, Mawasiliano, Mahakama, Maji, Nishati na shughuli za vijana.

Mkuu huyo ameongeza kuwa wakati wa ziara hiyo wananchi watapata fursa ya kuzungumza na rais kupitia katika mikutano ya hadhara iliyopangwa kila wilaya na kwamba majumuisho ya ziara yake itafanyika wilayani Bagamoyo Oktoba 9

Ametoa wito kwa wananchi mkoani humo kushiriki katika mapokezi ya rais na kuhudhuria kwa wingi kwenye mikutano ya hadhara na kuhakikisha amani na utulivu unakuwepo wakati wote wa mikutano hiyo.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa