Home » » Agro Forest yaanza kupanda miwa

Agro Forest yaanza kupanda miwa

KAMPUNI ya Agro Forest Plantation, mwishoni mwa mwezi huu inatarajia kuanza kupanda mbegu za miwa zitakazotumika kwenye mashamba mbalimbali mkoani Pwani.
Uamuzi huo umetokana na ombi lililotolewa na wenyeviti wa vijiji vya Kata ya Chumbi wilayani Rufiji, Mkoa wa Pwani walioitaka kampuni hiyo kuwekeza kwenye ardhi waliyowapa kwa ajili ya uwekezaji.
Akizugumza jijini Dar es Salaam, mmoja wa wakurugenzi katika Kampuni ya Agro Forest Plantation, Otieno Chaulo alisema wameshawaleta wataalamu waliobobea katika mashamba ya miwa pamoja na viwanda vya kutengeneza sukari.
Alibainisha kuwa wataalamu hao wanatoka nchini India na wameshatembelea eneo la mradi lililopo Rufiji na wamependekeza aina ya mbegu zitakazopandwa ambazo zitahimili udongo na hali ya hewa.
Aliongeza kuwa wataalamu hao watatu wamegawana katika makundi matatu, mmoja akiwa na uzoefu katika kutambua aina ya mbegu zitakazotoa sukari nyingi.
Otieno alisema mtaalamu mwingine ana ujuzi wa kutambua na kutibu miwa na wa mwisho ni mtaalamu wa ujenzi wa viwanda.
Alibainisha kuwa wataalamu hao wameshatoa mapendekezo ambayo yamekubaliwa na mwekezaji ambaye ni Agro Forest Plantation kwa ajili ya utekelezaji. Pia wametoa ushauri kwa serikali kusaidia kupeleka karibu miundombinu ya umeme pamoja na kuchonga barabara za mashamba ya wakulima wadogo wadogo wanaozunguka mashamba hayo.
Otieno pia alisema baada ya kupandikiza mbegu katika shamba la heka 500 mwishoni mwa mwezi huu, itachukua miezi 14 kustawi na kuotesha katika shamba la kuanzia heka 4,000 ambazo zitaweza kutoa miwa kwa ajili ya uzalishaji sukari.
Awamu ya kwanza ya uzalishaji sukari ambapo kiwanda kitategemea kuanza Oktoba 2015 ni tani 1,500 na kuendelea miaka inayofuata hadi kufikia tani 5,000 kama uwezo wake uliotathiminiwa katika uzalishaji sukari katika bonde hilo la Rufiji.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa