Home » » VIFAA 100 MAALUMU VYA KUBAINI KILEVI KWA MADERVA VYATUA PWANI

VIFAA 100 MAALUMU VYA KUBAINI KILEVI KWA MADERVA VYATUA PWANI

JESHI la Polisi mkoani Pwani limesema wamefanikiwa kupata vifaa vya kitaalamu vya kubaini vilevi na kwa sasa wameanza kutumia vipimo hivyo maalumu vya ulevi kuwabaini madereva wanaoendesha magari huku wakiwa wamelewa ama wametumia kilevi chochote kile wakati wakiwa kazini na kuwachukulia hatua za kisheria.

Kamanda wa Polisi mkoani humo Ulrich Matei amesema hayo kwenye kikao cha pamoja na wanahabari mkoani ambapo aliongeza kuwa tayari vipimo 100 vya ulevi vimesambazwa katika wilaya zote na lengo kuu ni kudhibitia ajali zinazotokea kwenye barabara kuu zinazotokana na ulevi wa madereva.

Matei amesema awali jeshi hilo lilikuwa na kipimo kimoja tu cha ulevi mkoa mzima hali ambayo ilikuwa ikiwawia vigumu kudhibiti ajali zitokanazo na ulevi ambavyo vimekuwa vikitokea katika maeneo kadhaa mkoani humo.

Aidha akizungumzia suala la usalama, Kamanda Matei amesema wameimarisha ulinzi ambapo wameanzisha mitaa 51 ya kiusalama mkoani humo na inaongozwa na viongozi wa serikali za mitaa ambao wanapaswa kuhakikisha wanatoa taarifa wakati wowote kwa viongozi wa jeshi hilo wilayani pale tu inapotokea ama kuhisi uwepo wa matishio ya uhalifu au uvunjifu wa amaani hivyo askari kuweza kuwahi eneo la tukio la kutatua tatizo husika.

Ameongeza kuwa tangu kuanzishwa mitaa hiyo 51 ya kipolisi Mkoa huo hivi sasa ni shwari na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano wa hali ya juu na wadau wa usalama ili kuliwezesha jeshi hilo kutekeleza majukumu yake ipasavyo kwani bila jamii shirikishi hakuna usalama wa kutosha.


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa