Home » » MAFIA - KISIWA CHA CHOLE CHAPATA UMEME

MAFIA - KISIWA CHA CHOLE CHAPATA UMEME

Shirika la Usambazaji Umeme Tanzania (TANESCO) limezindua rasmi umeme katika kisiwa cha Chole kilichopo kata ya Jibondo Wilayani Mafia kufuatia kukamilika kwa mradi uliotekelezwa kwa muda wa mwaka mmoja.

Mradi huo ulioanza kutekelezwa kuanzia Julai 2023 unatarajiwa kusambaza umeme katika visiwa vingine vilivyobaki vya Juani na Jibondo kwa hatua nyingine na kugharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 3.2 hadi utakapokamilika.

Akizungumza wakati wa uzinduzi, mgeni rasmi ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Mafia na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe. Omar Kipanga amemshukuru Mhe.  Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi.

" Tumshukuru Mhe. Rais kwa kukubali kutoa fedha pamoja na kuziimarisha taasisi zake ili kusimamia mradi huu" alisema Mhe. Kipanga. " Tunawashukuru pia TANESCO na Mkandarasi wetu kwa kusimamia vizuri mradi na kukamilika kwa wakati, inabidi tuwe walinzi wa kwanza wa miundombinu hii ya umeme ili itunufaishe sisi na vizazi vingine" alieleza.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha chole, Ndugu Ally Mgeni ameshukuru kwa hatua hiyo na kueleza umuhimu wa upatikanaji wa umeme kwa kuimarisha huduma za kiuchumi na kijamii zikiwemo Afya, na Elimu.

Lengo la mradi huo ni kuhakikisha kwamba kaya zaidi ya 1000 katika vijiji vyote vitatu vinaunganishwa umeme pindi  utakaposambazwa kote.

"Sasa hivi tunashukuru kwa kufika umeme kisiwani kwetu maana kabla ya kupata umeme tulikuwa na matatizo mengi, ila kwa sasa tunaamini biashara zitaongezeka na huduma za afya na shule zitakuwa vizuri, tunaishukuru sana Serikali kwa hatua hii" alisema mzee Halfani, mkazi wa kijiji cha Chole.

 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa