Home » » BUNGE LARIDHIA KUTIMULIWA KWA WAVAMIZI WA HIFADHI

BUNGE LARIDHIA KUTIMULIWA KWA WAVAMIZI WA HIFADHI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Mwandishi Maalum, Bagamoyo
Mwenyekii wa Kamati ya Kudumu ya Ardhi ,Maliasii na Utalii,Atashasta Ndetiye (katikati) akiongozana na wajumbe wengine wa kamati hiyo kutizama vyanzo vya maji vilivyoko katika Pori Tengefu la Loliondo. (Picha na Mtandao).
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii imeunga mkono uamuzi uliofikiwa na kamati maalumu iliyoundwa na serikali kwa ajili ya kutafuta suluhu ya kumaliza mgogoro wa ardhi baina ya Hifadhi ya Taifa ya Saadani na wananchi wa kitongoji cha Uvinje walioanzisha makazi ya kudumu ndani ya hifadhi kinyume cha sheria.
Kamati hiyo iliyoundwa na wajumbe watatu ambao ni Serikali ya Wilaya ya Bagamoyo, uongozi wa Kitongoji cha Uvinje na Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA) kupitia Hifadhi ya Saadani, ilifikia maazimio kuwwananchi wa kitongoji hicho walioanzisha makazi ndani hifadhi waondolewe kwa kulipwa fidia ili kumaliza mgogoro huo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana wilayani Bagamoyo, Mwenyekii wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii, Atashasta Ndetiye (pichani) alisema baada ya kutembelea eneo hilo, wamejiridhisha kuwa kitongoji hicho cha Uvinje kimeanzishwa ndani ya eneo la hifadhi ambapo ni kinyume cha sheria.
“Kiuhalisia tumeona kuna kitongoji ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Saadani, tumewasikiliza wananchi, tumesikiliza upande wa serikali, kwa mujibu wa taratibu na sheria wale wananchi wanapaswa watoe ushirikiano, tunaamini kuna taratibu za kiserikali zinafanywa kuhakikisha wale wananchi wanalipwa ili waondoke kwa usalama,” alieleza Ndetiye.
Aliongeza, “tumeona jinsi ambavyo baadhi ya wananchi hawako tayari kulipwa, lakini nadhani wakieleweshwa vizuri wataelewa kuwa ile ni hifadhi ya Taifa, na kama ni hifadhi ya Taifa basi inahusu maslahi ya Taifa, hivyo kila mwananchi anatakiwa atoe ushirikiano ili angalau serikali ifanye uwekezaji wa kueleweka.”
Ndetiye alisema kamati hiyo imeshaweka maazimio kwa ajili ya kulishauri Bunge ili liazimie ni nini kifanywe na serikali kumaliza mgogoro huo. Alisema, “Kwa udharura wake na kutokana na maelezo ya mkuu wa wilaya, kwa ujumla kamati inakubaliana nayo kwa sababu ameeleza vitu ambavyo tumeona vina tija zaidi kwa Watanzania na tunaenda kulishauri Bunge na serikali haraka iwezekanavyo ili hatua ziweze kuchukuliwa.”
Awali akielezea kuhusu mgogoro huo, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Majid Mwanga alisema baada ya maazimio ya kamati iliyoundwa na Serikali ya Wilaya kumaliza mgogoro huo, baadhi ya wananchi walikubali maazimio yaliyowekwa ya kulipwa fidia huku wengine wakikaidi kuondoka akiwemo mwekezaji aliyeshikilia sehemu ya eneo hilo kwa zaidi ya miaka tisa bila kuwekeza mradi uliokusudiwa ambao wamepewa kipindi cha mwezi mmoja waondoke kwa hiari kabla ya nguvu kutumika kuwaondoa.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Uvinje, Hussein Akida alisema kitongoji hicho kilianzishwa ndani ya Kijiji cha Saadani katika Wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani zaidi ya miaka 100 iliyopita huku kikiwa na ukubwa hekta 3,000 na mpaka sasa kina kitongoji hicho kina wakazi wasiopungua 70.
Aliiomba serikali kutambua mipaka ya kitongoji hicho pamoja na kuwasogezea wananchi huduma za kijamii. Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii walitilia shaka uwiano wa kimahesabu wa taarifa hiyo na uhalisia, na kuhoji iweje kitongoji chenye miaka mingi kiasi hicho kiwe bado hakijapewa hati ya kuwa kijiji kamili pamoja na idadi ndogo ya wananchi wasiongezeka ndani ya muda mrefu wa miaka zaidi ya 100 tangu kuanzishwa kwa kitongoji hicho.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Ramo Makani alisema mgogoro huo uko wazi na unapaswa kumalizika mara moja kwa kuwa Serikali ya Wilaya kupitia kamati iliyoundwa imeshafikia maazimio ya kuwaondoa wananchi walioanzisha makazi ndani ya eneo la hifadhi kinyume cha sheria. Alitoa mwito kwa wananchi kutii sheria za hifadhi na kuheshimu mipaka iliyowekwa kuepusha migogoro isiyo ya lazima baina ya serikali na wananchi.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa