Home » » PWANI WATAKIWA KUJITOKEZA KUPATA VITAMBULISHO

PWANI WATAKIWA KUJITOKEZA KUPATA VITAMBULISHO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
MKUU wa Mkoa wa Pwani, Mwantumu Mahiza, amewataka wakazi wa Mkoa wa Pwani kujitokeza kwa wingi kwenye usajili na utambuzi wa watu kwa ajili ya vitambulisho vya taifa.
Zoezi hilo ambalo linatarajiwa kuanza leo katika maeneo ya mkoa huo, linatarajiwa kufanywa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), ambapo viongozi kuanzia ngazi ya wilaya wametakiwa kutoa ushirikiano, ili kufanikisha zoezi hilo.
Mahiza alisema atahakikisha analisimamia vizuri zoezi hilo, ili liweze kufanikiwa, hivyo kuwaomba wakuu wa wilaya na wakurugenzi kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa kama serikali ilivyoagiza.
“Tunapaswa kuwapa NIDA ushirikiano, ninawaagiza viongozi wote wa mkoa huu muwapatie maelekezo watendaji waliopo chini yenu, pia mshiriki kutoa elimu kwa umma, kusimamia na kuendesha zoezi la usajili na utambuzi katika maeneo yenu ya utawala,” alisema Mahiza.
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa, Dickson Maimu, alisema zoezi hilo linaingia Mkoa wa Pwani baada ya usajili Zanzibar na Mkoa wa Dar es Salaam.
Maimu alisema mbali ya usaili, muda mwingi utatumiwa na watendaji kuhakiki taarifa za waombaji wa vitambulisho vya taifa, ili kuwa na taarifa sahihi za watu.
Mkurugenzi huyo aliishukuru serikali kwa kuwapatia fedha za kuendesha zoezi hilo, na kwamba watakapomaliza Mkoa wa Pwani watahamia katika mikoa ya Lindi, Mtwara, Morogoro, Tanga na Kilimanjaro
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa