Home » » WANAFUNZI 200 WASOMA KWENYE CHUMBA KIMOJA CHA DARASA

WANAFUNZI 200 WASOMA KWENYE CHUMBA KIMOJA CHA DARASA

WANAFUNZI 200 wamekuwa wakilazimika kubanana kwenye darasa moja wakati wa vipindi vya masomo katika shule ya Msingi Kongowe iliyopo halmashauri ya mji Kibaha kutokana na shule hiyo kukabiliwa na uhaba wa vyumba vya madarasa. Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Beatus Lingumbuka ameweka wazi hali hiyo wakati akielezea changamoto na mafanikio ya shule hiyo kwa waandishi wa habari waliofika hapo kujua sababu zinazopelekea idadi hiyo kubwa ya watoto kuminyana kwenye darasa moja. Amesema shule hiyo ina wanafunzi 1,502 kati yao wa kitengo cha watoto wenye ulemavu ni 42 idadi ambayo ni kubwa ikilinganishwa na madarasa yaliyopo hivi sasa. Mwalimu mkuu Lingumbuka amesema madarasa yaliyopo ni kumi lakini yanayotumika ni saba tu huku matatu yakiwa ni chakavu kwa miundombinu yake na hivyo kuifanya shule hiyo kuwa upungufu wa madarasa 14 kwa sasa ambayo ndiyo yatakayokidhi mahitaji kulingana na idadi ya wanafunzi waliopo hapo. Nae Diwani wa Kata ya Kongowe, ambae pia ni makamu mwenyekiti halmashauri ya mji Kibaha, Sloom Bagumeshi amesema atahakikisha anavalia njuga suala hilo ili kupunguza tatizo hilo na pia atazungumza na wapiga kura wake wachangie nguvu kazi na fedha huku akiitaka halmashauri na wadau wengine kushirikiana kuchangia ujenzi wa madarasa walau matatu ili kupunguza hali hiyo mapema. Hata hivyo, kuhusu uwepo wa idadi kubwa ya wanafunzi shuleni hapo , Bagumeshi amekiri ipo kinyume na miongozo ya Serikali inayoelekeza kuwepo wanafunzi 750 kwa shule moja hivyo inatakiwa kugawanywa na kuwa shule mbili kwani bila ya hivyo msongamano wa wanafunzi darasani hautakoma mapema.



0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Pwani Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa